Qurani
/
2- Surat AL - BAQARAH /
Introduction
(Imeteremka Madina na aya zake 286) Sura hii imeteremka Madina baada ya Hijra. Nayo ndiyo sura ndefu zaidi kuliko sura zote za Qurani Tukufu kwa mujibu wa utaratibu wa Msahafu. Sura hii imeanza kwa (kuchambua) kinaganaga yaliyohitimishwa na suratul Fatiha. Imeeleza kwamba Qurani ndiyo chanzo cha uongofu, na imewataja pia wale walioneemeshwa na Mwenyezi Mungu kwa radhi Yake na wale makafiri na wanafiki waliostahiki adhabu. Pia vile vile, sura hii imezungumzia ukweli wa Qurani na bila shaka ulinganio wa Qurani ni kweli. Kisha, sura imezungumzia juu ya aina tatu za watu: Waumini, makafiri na wanafiki. Imezungumzia juu ya ulinganio wa kumwabudu Mwenyezi Mungu Peke Yake na juu ya kutoa maonyo kwa makafiri na kutoa habari njema kwa Waumini. Kisha sura hii, imetaja habari maalum kuhusu Mayahudi (Bani Israili) kwa lengo la kuwaita ili warejee katika Njia ya Mwenyezi Mungu. Hapa, wamekumbushwa Siku za Mwenyezi Mungu (neema Zake) na mambo waliyoyafanya kwa Nabii Musa Amani ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake. Vilevile, wamekumbushwa juu ya Manabii Ibrahim na Ismail na vipi waliijenga Kaaba. Habari hizo za Bani Israili, zimechukuwa karibu nusu ya sura na ndani yake kuna mazungumzo yanayowakusudia Waumini kwa lengo la kuyazingatia yaliyotukia kwa Mayahudi na Wakristo. Baadaye, mazungumzo yameelekea kuwazungumzisha Waislamu kwa kuyataja mambo yaliyokubalika baina ya wafuasi wa Musa na wafuasi wa Muhammad kati ya fadhila za Ibrahim, uongofu wake, ukoo wake na kutaja suala la kibla na mengineyo. Kisha, sura imezungumzia juu ya tawhid (kumpwekesha Mwenyezi Mungu) na kukumbushia kwa Alama za Mwenyezi Mungu zinazobainisha kuwepo Kwake. Imetaja shirki, vyakula vilivyoharamishwa na kwamba kuharamisha na kuhalalisha ni Haki ya Mwenyezi Mungu Peke Yake. Pia vile vile, sura imebainisha vyanzo vya wema na baadhi ya hukumu za kufunga saumu, wasia, kula mali za watu kwa njia zisizofaa, hukumu za kisasi, kupigana vita, kuhiji, ulevi, kamari, kuoa, talaka, kunyonyesha, eda na mengineyo. Aidha, sura hii, imezungumzia itikadi za kiujumla kama utume, tawhid na kufufuliwa. Kadhalika, sura imezungumzia juu ya utoaji (mali), riba, kufanya biashara na kuandika deni. Kisha, sura imehitimishwa kwa dua ya Waumini kwa Mola wao Awasaidie na Awatilie nguvu. Sura hii imejumuisha nguzo mbalimbali. Miongoni mwa nguzo hizo ni: * Kufuata Njia ya Mwenyezi Mungu na kuitekeleza ipasavyo dini Yake. Haya ni mambo mawili yenye kuleta furaha kwa mwanadamu duniani na akhera na kwamba haifai kwa mtu mwenye akili kuwalingania wengine wafanye wema na fadhila wakati ambapo yeye mwenyewe anajisahau nafsi yake. Pia, ni lazima mwanadamu ayashindanie ya kheri na siyo maovu, na ayapandishe cheo mambo ya fadhila siyo mambo mabaya. * Misingi ya dini ni mitatu nayo ni: Kumwamini Mwenyezi Mungu, kuamini kufufuliwa na kufanya vitendo vizuri. * Thawabu, hutegemea kuamini pamoja na vitendo na kwamba sharti ya kuamini ni utiifu wa kinafsi na unyenyekevu wa kimoyo kwa yote aliyokuja nayo Mtume (S.A.W) na kwamba wasiyo Waislamu hawatawapenda Waislamu mpaka Waislamu waifuate dini yao. * Mamlaka kuu ya sheria, ni lazima iwe mikononi mwa Waumini waadilifu na wala siyo mikononi mwa makafiri na madhalimu. Pia, kuiamini Dini ya Mwenyezi Mungu kama Alivyoiteremsha, kunahitajia umoja na mapatano kwani kuliacha hilo, kunaleta hitilafu na utengano. Aidha, kutimiza malengo makubwa, kunahitaji mwanadamu awe na subira na kushikamana na sala. Kadhalika, kuiga bila kupima, si jambo zuri kwa kuwa huleta ujinga na wahaka. * Mwenyezi Mungu Amewahalalishia waja Wake vyakula vizuri na Amewakataza vitu vibaya vichache. Hakuna ruhusa kwa mtu yeyote kuhalalisha au kukataza isipokuwa Mwenyezi Mungu tu na kwamba katika hali ya dharura, kuna ruhusa (kula) vitu vilivyokatazwa. Hii ni kwa mujibu wa kanuni isemayo: Wakati wa dharura huruhusiwa yaliyokatazwa. Dharura hukadiriwa kwa kiasi chake. Vile vile, dini imejengwa juu ya urahisi na kuepusha dhiki na taabu, kwani Mwenyezi Mungu Hailazimishi nafsi yoyote kufanya jambo isiloliweza na wala Mwenyezi Mungu Hawaamuru waja Wake ila kwa lile waliwezalo. Kadhalika, kuitia nafsi katika maangamizo ni haramu na haifai. Aidha, mambo hutafutwa kwa sababu zake na njia maalum zinazopelekea kufanikishwa. Pia, ni marufuku kuwalazimisha watu kuingia katika dini yoyote. Vile vile, kupigana vita (kumetungiwa sheria) katika Uislamu kwa ajili ya kujilinda, kudhamini uhuru wa dini na kuulinda utawala wa Kiislamu katika jamii yake. * Kila Mwislamu ana haki ya kulitafuta fungu lake duniani, wakati huo huo akitekeleza majukumu yake ya akhera. Aidha, kufunga milango ya maovu na kufungua milango ya wema, ni miongoni mwa malengo ya sheria ya Kiislamu. * Kuamini na kusubiri, ni sababu za kushinda wachache waadilifu dhidi ya wengi madhalimu. Vile vile, kula mali za watu kwa njia isiyo ya haki, ni haramu na kwamba mwanadamu atalipwa kwa mujibu wa vitendo vyake na wala siyo kwa vitendo vya mwingine. Kadhalika, hekima ya sheria ya Kiislamu anaifahamu mwenye akili nzuri kwa kuwa ina ukweli, uadilifu na manufaa kwa watu.
Main Page
Contact us
Links
About us
Site Map